Waziri wa Maliasili na Utalii, Mhe. Angellah Kairuki (Mb) ameshuhudia makabidhiano ya vifaa vya awali kati ya Makumbusho ya Taifa la Tanzania na Makumbusho ya Sultani ya Oman, vitakavyotumika kwa ajili ya kuhifadhia mikusanyo mbalimbali iliyopo katika  Makumbusho ya Tanzania.

Makabidhiano hayo yamefanyika leo tarehe 6 Februari 2024 katika Kituo cha Makumbusho na Nyumba ya Utamaduni kilichopo Posta jijini Dar es Salaam.

 


Awali, akizungumza na Ujumbe wa Wataalamu kutoka Makumbusho ya Sultani ya Oman na Makumbusho ya Taifa la Tanzania, Mhe. Kairuki ameushukuru ujumbe huo kwa kuweza kuleta baadhi ya vifaa vya awali ikiwa ni mwanzo mzuri wa kutekeleza Mkataba wa Mashirikiano baina ya Makumbusho ya Taifa la Tanzania na Makumbusho ya Sultani ya Oman.


Kufuatia hatua hiyo, Mhe. Kairuki ameahidi pamoja na mambo mengine kuvionyesha baadhi ya vifaa vya kiutamaduni vya Sultani ya Oman katika Makumbusho ya Taifa la Tanzania ili watu waweze kujua na kujifunza utamaduni wa Oman.




OMAN NA TANZANIA ZAKABIDHIANA VIFAA VYA UHIFADHI WA MIKUSANYO YA KIMAKUMBUSHO 

Na Happiness Shayo- Dar es Salaam

Waziri wa Maliasili na Utalii, Mhe. Angellah Kairuki (Mb) ameshuhudia makabidhiano ya vifaa vya awali kati ya Makumbusho ya Taifa la Tanzania na Makumbusho ya Sultani ya Oman, vitakavyotumika kwa ajili ya kuhifadhia mikusanyo mbalimbali iliyopo katika  Makumbusho ya Tanzania.

Makabidhiano hayo yamefanyika leo tarehe 6 Februari 2024 katika Kituo cha Makumbusho na Nyumba ya Utamaduni kilichopo Posta jijini Dar es Salaam.

Awali, akizungumza na Ujumbe wa Wataalamu kutoka Makumbusho ya Sultani ya Oman na Makumbusho ya Taifa la Tanzania, Mhe. Kairuki ameushukuru ujumbe huo kwa kuweza kuleta baadhi ya vifaa vya awali ikiwa ni mwanzo mzuri wa kutekeleza Mkataba wa Mashirikiano baina ya Makumbusho ya Taifa la Tanzania na Makumbusho ya Sultani ya Oman.

Kufuatia hatua hiyo, Mhe. Kairuki ameahidi pamoja na mambo mengine kuvionyesha baadhi ya vifaa vya kiutamaduni vya Sultani ya Oman katika Makumbusho ya Taifa la Tanzania ili watu waweze kujua na kujifunza utamaduni wa Oman.

Aidha, Mhe. Kairuki ametumia fursa hiyo kumshukuru Mtendaji Mkuu wa Makumbusho ya Sultani ya Oman, Mhe.  Jamal bin Hassan Al Moosawi kwa kukubali ombi maalum la ujenzi wa jengo litakalokuwa Kituo cha Kiutamaduni cha  Kiswahili na Oman.

Waziri Kairuki ametoa wito kwa wataalamu wa pande zote mbili za Tanzania na Oman kuweka juhudi katika kuratibu mradi huo vizuri na kuhakikisha malengo yaliyowekwa yanafikiwa.

Naye, Mkurugenzi Mkuu wa Makumbusho ya Taifa la Tanzania, Dkt. Noel Lwoga amesema kikao hicho kimejikita katika kuainisha maeneo ya kuweka mradi wa jengo la kiutamaduni la Kiswahili na Oman, kupitia eneo ambalo litakwenda kuboresha Onesho la Historia nchini, kupitia mikusanyo yote ambayo ina viashiria vya mashirikiano baina ya  Oman na Tanzania ili kuviainisha vinahitaji uhifadhi wa aina gani, vinaweza vikaoneshwa namna gani kule Oman na nchini Tanzania.

Tanzania na Oman zilisaini Mkataba wa Makubaliano (MOU) Juni 13, 2022 na baada ya majadiliano ya muda mrefu Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki iliwezesha kufanyika kwa mkutano wa kwanza wa pamoja baina ya Makumbusho ya Tanzania na Makumbusho ya Sultani ya Oman jijini Dar es Salaam kuanzia  Oktoba 6 hadi, 8 2023 ambao ulihitimishwa kwa kusaini makubaliano yaliyolenga katika Usimamizi wa Mikusanyo, Uhifadhi wa Mikusanyo, kufanya Tafiti, Maonesho ya pamoja na programu za uhamasishaji.